Mmmmmh… Mambo mengine ni mazito kusimulia , ila itatubidi tuambizane , huenda ikawa sababu ya kumuokoa mtu, la! Mtu itakuwa ni kwa uchache mno, liwaokoe watu, maana wapo wengi waliolivalia njuga na kukosa haya. Dunia imepasuka mahali kama wasemwavyo wengine, Nani ataziba kiraka au kama ni ufa halikadhalika? Maana, usipoziba ufa utajenga ukuta.Wapo wengine walosema, wameabiri basi la dunia lakini lipo kasi mno, wakamrai konda na dereva wakiegesha sehemu , wawashushe ! Maana dunia iko kasi mno. Fikra zao zinawapa taswira ya dunia jinsi ilivyo, sijui mimi na wewe tunaiwazia nini au kuchelea lipi katika safari yetu ya maisha na hatima yake. Kilele kitafika na tutaiaga dunia, Hilo halina shaka, lakini kwa sasa hivi tutaishije? Wahenga walisema, ukiishi na Mtu wa bunduki, utakufa na Mtutu wa bunduki, hivyo basi ni bora kubadili mienendo kabla hayajakukuta ya kukuta. Kama asemavyo msanii mmmoja wa kuchekesha kule Tanzania kwa jina la Tabu Mtingita, ‘ Aaasubuutu..kitamkuta Mtu kitu hapa, anakufa mmoja wallahi, umetindinganya mambo, ungenisikiliza , usingeyatondomoa (usingeyaharibu).’
Sasa hebu tega sikio, macho yakodoe kodo, akili yako, nafsi, hisia zako zote pamoja na kiwiliwili ziandamane nami. “Mke wa Mtu Sumu” Ni kauli inayosemwa mno , imezoeleka sana , mpaka watu wanaichukulia ni ya kawaida mno. Sisi vijana husema kwa dhihaka, ‘kama mke wa mtu sumu tutamnywa na maziwa’ , yaani sumu kiboko yake maziwa, ndio huduma ya kwanza kwa mtu aliyekunywa Sumu. Lakini wengi wanakosea mno, sio kila neno linalosemwa lina haki ya kulidhihaki, mengine iko haja ushike sikio na kujiuliza maswali mengi, uwatake wakubwa na ushauri na ulipe jambo Hilo mazingatio.
Maana yake kubwa msemo huu ni; Haifai kwa mtu kutembea na mwanamke wa mtu ambaye ameolewa kisheria. Bibilia imeandika, ‘Mwanamke mpumbavu huivunja ndoa yake kwa mikono yake mwenyewe.’ Lakini haikunuia kumuelimisha au kumuonya mwanamke pekee, hata mwanamume mpumbavu halikadhalika huvunja ndoa yake kwa mikono yake mwenyewe. Zinaa ya watu walio katika ndoa ina uzito mkubwa mno, ndio maana hata katika Kitabu cha Korani tukufu, hukmu iliyotolewa na Mungu kwa Vijana ambao hawajaoa wanapofanya tendo la zinaa , ni kupigwa bakora themanini, ilhali kwa wale wanandoa wanapozini, hukmu Yao ni kupigwa mawe mpaka kufa , hukumu nzito, kwa uzito wa jambo lenyewe. Dhambi inapokithiri , watu hutaka kuhalalisha yaliyoharamishwa na kuyafanya yaonekane kawaida, ilhali ni kinyume na uhalisia wa mambo.
Wapo wanawake wengi ambao japo wameolewa , huwaendea kinyume waume zao na kutoka ndani ya ndoa Hadi kufanya mapenzi na wanaume tofauti na wale waliowaoa, cha kushangaza zaidi, wengi wao utawakuta wameivua Pete wakificha wasijulikane kwamba ni wake za watu. Wanajitongozesha na kuapa kabisa kwamba hawajaolewa, ama kutoa Siri za chumbani kutafuta sababu za kufanya uchafu na kutembea na wanaume wengine.
Wanaume wanapenda na kujawa na matanio tu kwa kumuona mwanamke, anapomuuliza mwanamke na akakiri kwamba hajaolewa ni rahisi kwake kujenga mahusiano ya kimapenzi nae iwapo ametokea kumpenda au kutamani muonekano wa mwanamke huyo, unafahamu fika hasi na chanya Ndizo zinazoungama, ukimuekea mbuzi nyasi azilinde, ukija zimeliwa wala usimuulize zimekwenda wapi. Na vilevile Wapo aina ya wanaume na vijana wanaojitapa kifua, kwa kutaka kutembea na wake za watu , hawatongozi ila wanawake ambao wameshaolewa , wakijidai ndio mafundi wanaokarabati wafikishe magari mbele ya safari ambako pengine walioko katika ndoa hawafiki.
Wala hili siliamini, ni ufuska tu uliojikita katika nyoyo za watu, wamejizoeza tabia chafu, ni watu aina yake lakini, wana mshipa flani wa uzinzi ndani Yao, wewe mwanamke unataka nini zaidi ya stara uliyoipata katika ndoa? Vipi uzurure ukijinadi kwamba hujaolewa ilhali ni Mke wa mtu? Watu wamekosa haya, na ndio maana wengi wanatembea barabarani nusu uchi wala habari hawana. Kwa hali hii tunataraji tukimuomba Mungu atusikie? Na pia atuepushe na majanga kama hili janga la maradhi ambukizi ya Corona?
Dhambi zikikithiri ndio maisha yanakuwa magumu mno na wanadamu tunanyanyasika , hebu turudini kwa Mungu na tubadili tabia zetu. Majuzi kuna bwana mmoja alifanyiwa Kitendo cha unyama mno ambacho wala hakisemeki, kinakirisha mno, na visa vingi kama hivyo vimefanywa kwa watu wanaotembea na wake za wenyewe. Kijana mwenzangu, au mwanaume mwenzangu, iwapo mwanamke yuko katika ndoa na hajiheshimu, ni jukumu Lako wewe kuwa imara na kumuepeka , kutokuwa na mahusiano yoyote ya kimapenzi.
Wanasema malipo ni hapa duniani, na dhambi la zinaa linalipa hadi vizazi saba vya ukoo wa mtu. Ukitembea na mke wa mtu ukajiona kidume, amini utalipwa na mkeo, au mwanao, mamako, Shangazi yako, dadako, mjukuu wako, almuradi aibu ikufike ujihisi uchungu kama alivyohisi huyu uliyetembea na mkewe. Mke yu uchungu, kweli sikatai, na anauma mno achukuliwapo na mwengine na mwenyewe ukeli hai, hukutia majonzi ukawa hujifai, usipokuwa makini ukazirai, na maishani ukakosa kufurahi. Wanaume wengi wanapojua kwamba wake zao wanawaendea kinyume huwapa talaka na kubaditilisha ndoa, wengine huwapiga wanawake nusura kuwaua, wengine kwa kushindwa kujizuia wakawaua wake zao na watoto na kujiua wao wenyewe pia, zote ni hasira za mke kutoka nje ya ndoa. Mtu hufikiria Mali alizotoa na Fadhila alizompa mwanamke huyo ndani ya ndoa kama Mzazi mwenzake akashindwa kuelewa chanzo cha kukosewa kiasi kikubwa mno.
Majuzi kijana mmoja alietembea na mke wa mtu mara si moja alifuatwa na mume wa Yule mwanamke aliyetembea nae,alikuwa yupo kwenye stendi anapofanya kazi yake ya bodaboda, baada ya mazungumzo ya muda kuhojiwa kuhusu kutembea na mke wa Yule bwana, kijana alikana, lakini baada ya kutishwa, kushurutishwa na kuonyeshwa hadi ushahidi wa picha na meseji kwenye simu ya mwanamke Yule, kijana hakuwa na budi kukubali. Kwa ustaarabu yule mdhulumiwa akamuomba waondoke sehemu kando kidogo ambapo wangekwenda kuongea na kuelewana au la sivyo amuanzishie mtiti palepale na aieleze halaiki kuwa kijana huyo alikuwa anatembea na mkewe, kwa hali hio hata ukitiliwa na kelele ya Mwizi watu watakuvamia, kukufakamia juu kwa juu,na kukupiga kitutu kama Mbwa aliyeingia msikitini, ilimradi wakunyooshe na kukutia adabu ili usirudie kosa lako. Basi kwa uamuzi wa busara kijana aliongozana na bwana aliyekuwa akimla uroda mkewe ambaye alihitaji faragha Yao wawili. Walipofika katika jengo alioelekezwa , mijanadume kama Tisa ilitokeza na kumkamata akashindwa kujitetea, watu hao wakamfanya mwanamke au wakamuingilia ambapo Hilo ni kinyume na maumbile, kijana akapiga kelele bila msaada wowote ila baadae wakaja kumsaidia kutoka katika sehemu ile aliyokuwa.
Kwa kisa hiki nilijifunza mengi, kikanichukiza mno, haijuzu kulipa ubaya kwa ubaya, makosa mawili hayatengenezi walau jema moja, halafu hili lilikuwa dhambi kubwa mno. Tumesikia watu wamekwama na kugoma kutoka katika tendo la ndoa baada ya kutembea na mke wa mtu, wengine wakawekewa tego na kubaki na uvimbe katika sehemu zao za korodani, na Kuwa na mapumbu , au wengine wakarogwa na wanaume wenzao na kuwa wendawazimu , au kufanya mashine zikate moto, au hata kuuwawa kwa kutembea na mke wa mtu.
Hizi ndio Zile Sumu tunazoambiwa; ‘Mke wa mtu sumu.’ Hebu tuweni na staha na tujitathmini, kufanya kosa si kosa, lakini kurudia kosa ndio kosa, Leo tuakifike na wake za watu, naamini kama walivyosema wahenga; Mui huwa mwema. Tubadilisheni mieneno na tuweni bora wa tabia. Ama kwa hakika; Mke wa mtu siku zote atabaki kuwa sumu.
Comments
Excellent Article.
Excellent Article.